Burundi yaafiki na Tanzania kuwarejesha wakimbizi wote nyumbani

Burundi imesema imekubaliana na Tanzania kuwarejesha wakimbizi wote nchini Burundi kutoka Tanzania, watake wasitake. Hata hivyo, serikali mjini Bujumbura imelishutumu shirika la UNHCR kuwa kikwazo kwa mpango huo.
   Tansania Flüchtlinge aus Burundi Cholera (Getty Images/AFP/D. Hayduk)
Serikali ya Burundi imelishutumu Shirika la Wakimbizi la Umoja wa Mataifa, UNCHR, kwa kuwa kikwazo kwenye mchakato wa kuwarejesha nyumbani wakimbizi wa nchi hiyo walioko katika taifa jirani la Tanzania, huku ikisema kuwa imekubaliana na serikali ya Tanzania kuwarejesha nyumbani wakimbizi elfu mbili kila wiki, kwa namna yoyote ile. 
Katika mkutano na waandishi wa habari baada ya ziara iliyomfikisha katika kambi za Nduta na Mutenderi nchini Tanzania, Waziri wa Mambo ya Ndani wa Burundi, Pascal Barandagiye, anasema wamegunduwa ya kuwa shirika la UNHCR limekuwa likizichonganisha serikali za Tanzania na Burundi:
Burundi Pierre Nkurunziza, Präsident (picture-alliance/AP Photo/B. Mugiraneza)
Pierre Nkurunziza, Rais wa Burundi
"UNCHR walipoulizwa na serikali ya Burundi kwa nini wakimbizi wanaorejea nchini ni idadi ndogo, walijibu kuwa hao ndio serikali ya Tanzania iliyoweza kuwaorodhesha. Na serikali ya Tanzania ikiuliza kwa nini wanarejea wakimbizi kwa kiwango hicho, wanajibu kuwa serikali ya Burundi imependelea hivyo kwani haina uwezo wa kuwapokea. Hivyo tumegunduwa UNHCR inazichonganisha serikali hizi mbili. Na ni kikwazo kwa mchakato wa kurejea wakimbizi nchini." Amesema Barandagiye.
UNHCR yashutumiwa kuwatenga wawakilishi wa serikali
Waziri huyo amesema wawakilishi wa makambi hayo ambao wanaiwakilisha pia serikali wamekuwa wakitengwa na shirika hilo, huku kukiwa na wakimbizi 15,000 wanaoishi bila kuorodheshwa ndani ya makambi hayo.
Hata hivyo, serikali za Burundi na Tanzania zimeafikiana kuwarejesha wakimbizi 2,000 kila wiki, operesheni itakayoanza kutekelezwa tarehe Mosi mwezi ujao wa Septemba:
Barandagiye ameongeza kusema, "Serikali ya Tanzania na sisi tuna mtazamo mmoja. Tumeafikiana ifanyike kwanza sensa ya wakimbizi waliosalia katika kambi hizo na wakuu wa kambi washirikishwe. Hata serikali ya Tanzania iliwaambia hakuna sababu za kubaki nje ya nchi wakati nchini kwao kuna amani, labda wawe na mipango mingine. Ardhi ile ina wenyewe ambao ni Watanzania. Tutawarejesha hadi Desemba 31 kutakuwa hakuna mkimbizi aliyabaki."
Nani atagharimia mchakato huo?
Changamoto kubwa ni kuwa shirika la UNHCR linalogharia kifedha mchakato wa kuwarejesha nyumbani wakimbizi halijashirikishwa katika makubaliano hayo ya kuwarejesha wakimbizi bila hiari yao, lakini wakati huo huo serikali ya Burundi ikilitaka kutimiza wajibu wake.
Mnamo mwezi Machi mwaka 2018, yalisainiwa makubaliano ya pande tatu kati ya serikali za Burundi, Tanzania na UNHCR ili kuwarejesha nyumbani wakimbizi wanaokadiriwa kufikia laki mbili kwenye makambi nchini Tanzania.

Post a Comment

0 Comments