Serikali yatoa neno kuhusu kuwawezesha Mawakala wa Mbegu za Kilimo


Upatikanaji wa mbegu bora zikiwemo za mahindi ngano, maharage, mpunga, soya, alizeti, mtama, ufuta, viazi mviringo na mbegu za mazao ya bustani kwa msimu wa 2018/19 ulifikia tani 49,040 kati ya hizo tani 38,507 sawa na asilimia 78.6 zilizalishwa nchini na tani 8,361 sawa na asilimia 17 ziliagizwa nje ya nchi na tani 2,171 sawa na asilimia 4.4 ni bakaa ya msimu wa 2017/2018.

Naibu Waziri wa Kilimo Mhe Hussein Bashe ameyasema hayo leo, Septemba 12, 2019 wakati akijibu swali la Mbunge wa Kasulu Mjini Mhe Daniel Nsanzugwanko mkakati wa serikali katika kutatua uhaba mkubwa wa mbegu hasa za mahindi na maharage ambayo ni mazao ya chakula na namna ambavyo serikali itajikita katika uzalishaji wa mbegu.

Alisema kuwa Mikakati ya Serikali ya kuongeza uzalishaji wa mbegu ni pamoja na kuwezesha Wakala wa Mbegu za Kilimo (ASA) kuongeza uzalishaji wa mbegu bora katika mashamba ya Mwele, Dabaga, Mbozi, Msimba, Bugaga na Arusha; kutumia Taasisi za Utafiti wa Kilimo kuzalisha mbegu mama, msingi na zilizothibitishwa ubora na kukodisha maeneo katika mashamba ya ASA kwa kampuni binafsi za mbegu ili kuongeza uzalishaji wa mbegu bora za mazao mbalimbali ikiwemo mahindi na maharage.

Aidha, mikakati mingine ni kuongeza eneo la umwagiliaji katika mashamba ya mbegu ya Msimba, Arusha, Dabaga na mashamba ya Vituo vya Utafiti kutoka hekta 200 hadi 600; kushirikisha taasisi za umma kama Jeshi la Magereza na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) kuzalisha mbegu bora pamoja na vikundi vya wakulima wadogo kuzalisha mbegu za Daraja la Kuazimiwa ubora.

Mhe Bashe alisema kuwa shamba la mbegu la Bugaga lililopo katika Wilaya ya Kasulu lina ukubwa wa hekta 200. Shamba hilo linamilikiwa na ASA na kwa sasa linatumika kuzalishia mbegu bora za mahindi, maharage na alizeti. Aidha, shamba hilo linatumika kuzalisha miche bora ya michikichi, miche ya matunda ya machungwa na maembe.

Pia serikali imeanza kuchimba kisima cha maji katika shamba hilo ili kuwezesha uzalishaji wa mbegu kwa kipiti chote cha mwaka. Vilevile, ASA imejenga kitalu nyumba cha kukuzia miche ya chikichi pamoja na kuandaa bustani ya kukuzia miche hiyo ya michikichi na miche ya matunda.

Aliongeza kuwa Mkakati wa Serikali ni kuongeza uzalishaji wa mbegu ambapo Serikali katika mwaka wa fedha 2019/20 imetenga takribani shilingi bilioni 13 kwa ajili ya utafiti wa mbegu kupitia Taasisi ya Utafiti wa Mbegu-TARI na uzalishaji wa mbegu kupitia Wakala wa Mbegu za Kilimo –ASA kwa ajili ya kuzalisha mbegu kwa njia ya umwagiliaji ili kuongeza uzalishaji mara tatu hadi nne zaidi ya sasa. "Aidha, nitumie fursa hii kuzisihi halmashauri kutotumia maeneo yaliyotengwa kwa tafiti za kilimo kwa shughuli zingine ikiwemo kujenga stendi za mabasi" Alikaririwa Mhe Bashe

Kadhalika, Wizara ya Kilimo itaamua kuyaachia maeneo hayo kwa shughuli zingingine baada ya kujiridhisha kwamba maeneo hayo hayana tija kwa shughuli hizo za kilimo.

Naye Naibu waziri wa Kilimo Mhe Omary Mgumba akijibu swali la mbunge wa viti maalum Zaynab kuhusu serikali kutafuta soko la zao la nazi alisema kuwa Soko la kudumu la zao la nazi lipo nchini kwa sababu kiasi cha nazi kinachozalishwa bado hakikidhi mahitaji ya soko la ndani ya nchi kutokana na kuongezeka kwa matumizi ya zao hilo ikiwemo ulaji wa madafu na watumiaji wa nazi.


Aidha, mafuta mwali yanayotokana na nazi yanaendelea kupata umaarufu kutokana na uhitaji wake kuwa mkubwa ndani na nje ya nchi, ambayo lita moja inafika hadi Shilingi 40,000/=. Bidhaa kama fagio, mbao, kamba na samani zinazotokana na mti wa mnazi na uwezo wa zao hilo kutunza mazingira huongeza thamani ya zao la minazi.

Alisema kuwa Katika kuimarisha soko la zao la nazi nchini msimu wa mwaka 2018/2019 wakulima wapatao 74 katika mikoa ya Lindi na Mtwara wamefundishwa namna ya kukamua mafuta mwali.

Vilevile, kikundi cha wanachama 50 katika Wilaya ya Bagamoyo kimepewa mashine yenye uwezo wa kukamua lita 500 za mafuta mwali kwa mwaka. Aidha, Serikali inaendelea kuimarisha masoko ya mazao yote ya kilimo likiwemo zao la nazi kwa  kuwaunganisha wakulima na wanunuzi kupitia vyama vya ushirika, masoko ya moja kwa moja na viwanda vidogo  vya kuongeza thamani ya zao la nazi.

Mhe Mgumba amesema, Serikali inaendelea kutoa elimu kwa wazalishaji wa zao la nazi kuendelea kupanda mbegu bora zenye ukinzani dhidi ya magonjwa na zenye tija  kubwa. Tanzania ni nchi ya kumi duniani kwa uzalishaji wa nazi ikiongozwa na nchi ya Indonesia na kwa Afrika ni nchi ya kwanza ambapo huzalisha wastani wa tani 530,000 za nazi kwa mwaka ikifuatiwa na Ghana ambayo huzalisha wastani wa tani 366,183.

Aidha, Serikali inaendelea kuhamasisha kilimo cha minazi nchini ambapo imeanzisha shamba lenye ukubwa wa hekta 54 katika kituo kidogo cha utafiti cha Chambezi Wilaya ya Bagamoyo ili kuzalisha miche bora  ya minazi yenye ukinzani dhidi ya ugonjwa wa kunyong’onyea kwa minazi (Coconut Lethal Disease) na kuisambaza kwa wakulima kwa gharama nafuu.

Aliongeza kuwa Serikali inahamasisha kilimo cha minazi katika maeneo mapya ili kuongeza uzalishaji wa nazi nchini ambapo msimu wa 2018/2019 ilizalisha na kusambaza jumla ya mbegu 11,000 kwa wakulima katika mikoa ya Rukwa na Mwanza. Aidha, Serikali inafanya mazungumzo na Jumuiya ya Asia - Pasific Coconut Community (APCC) ambayo hutunza “germplasm” ya minazi kuwezesha upatikanaji wa mbegu bora za minazi zenye kuongeza tija kwa wakulima

Post a Comment

0 Comments