Alichosema IGP Sirro kuhusu uchaguzi Mkuu 2020


Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini IGP Simon Sirro, anaendelea na ziara katika mikoa yote nchini kwa lengo la kukagua na kuona maandalizi ya Jeshi la Polisi pamoja na kamati za Ulinzi na Usalama kuelekea Uchaguzi Mkuu mwezi Oktoba mwaka huu.

Aidha amewataka wananchi ambao ni washtakiwa au wafungwa wanaopata msamaha wa Rais kutoka gerezani, kuacha kujiingiza katika matukio ya uhalifu jambo ambalo ni kinyume na sheria za nchi.

IGP Sirro amesema hayo akiwa kwenye ziara ya ukaguzi mkoani Singida ambapo alizungumza na Polisi Kata waliopo kwenye mkoa huo na kuwataka kuendelea kushirikiana na wananchi katika mapambano dhidi ya uhalifu ikiwa pamoja na kutoa elimu kwa wananchi kuacha kujiingiza kwenye matukio ya uhalifu hususan wa kutumia silaha za moto.

Aidha, IGP Sirro amesema kuwa, wenyeviti wa kamati za Ulinzi na usalama za wilaya na mikoa kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi na kwamba hadi kufikia sasa hali ya usalama nchini imeendelea kuwa shwari.

Naye kamanda wa Polisi mkoa wa Singida Sweetbert Njewike amesema kuwa, hali ya usalama katika mkoa huo inaendelea kuwa shwari na kwamba matukio ya uhalifu yamepungua kutokana na ushirikiano mkubwa unaotolewa na wananchi pamoja na wadau wengine.

Bofya hapa kusoma Habari zote

Post a Comment

0 Comments