Amber Lulu Mahaba Hadharani, Ajiachia kwa Diamond


SIKU zote ukistaajabu ya Musa utayaona ya Firauni! Hicho ndicho kinachotokea kwa staa wa kike wa Bongo Fleva, Lulu Auggen ‘Amber Lulu’ ambaye ameshindwa kujizuia na kuangushia penzi lake kwa mwanamuziki Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’.

Amber ameeleza waziwazi hisia zake za kimapenzi kwa Diamond au Mondi ambaye ni bosi wa Lebo ya Wasafi Classic Baby (WCB).

Amber amesema Mondi anamnyima kabisa usingizi kutokana na jinsi ambavyo moyo wake umemdondokea kimahaba.

Amber  ameamua aweke wazi hisia zake kwani haoni kama kuna tatizo kueleza ukweli juu ya kumpenda mwanamuziki huyo.

Amesema anaiona hatua hiyo kuwa ni nzuri kwa sababu anakua, ametoa kile kilicho ndani ya uvungu wa moyo wake.

“Unajua watu ambao siyo waelewa, ndiyo wataumiza vichwa na kunishangaa, lakini ukweli ni kwamba, nimempenda na ninavyoona hali inazidi kunishika, nimebidi nitoe la moyoni mwangu ili nisije kufa nalo,” alisema Amber anayekimbiza na wimbo wake wa Jini Kisirani.

Mrembo huyo alisema kuwa, watu wasiwe wanafiki kushangaa alichokisema, kwani kuna mwanamke gani ambaye havutiwi na mwili wa Mondi, sema ndiyo hivyo watu hawawezi kuongea yaliyopo mioyoni mwao.

Amber aliendelea kusema kuna wakati mtu anashindwa kabisa kueleza hisia zake za moyoni, hivyo anaamua tu kuweka wazi kupitia mitandao ya kijamii na ujumbe unamfikia mlengwa.

“Sitaki kuwa muongo au kufa na kitu rohoni kwangu, habari ndiyo hiyo.

“Kiukweli ninamzimikia mno na naona bora nimesema, labda anaweza kunifikiri kuliko wale ambao wanaumia na hali zao mioyoni, kwani ni mbaya,” alisema Amber akisisitiza kuwa yupo tayari kuziba nafasi iliyoachwa na Tanasha Donna kwa Mondi.

Mwanadada huyo mwenye umbo matata alisema, mtu yeyote hasa wanawake waliowahi kuwa na uhusiano naye au hata kuzaa naye, wasimchukulie tofauti, kwani kila mbuzi hula kwa urefu wa kamba yake.

“Najua wanawake wa Mondi watanibinulia midomo, lakini watambue kwamba siku zote kila mbuzi anakula urefu wa kamba yake.

“Mimi watakavyonichukulia poa tu, ila tu siyo kwa mwili ule, tamaa imenishika vibaya sana,” alisema Amber ambaye aliposti picha ya Mondi kwenye ukurasa wake wa Mtandao wa Instagram.

Huko nyuma, Amber amewahi kutajwa kutoka kimapenzi na wasanii kama Young D na Prezzo wa Kenya.

Post a Comment

0 Comments