China yatoa radiamali kufuatia madai ya Uingereza kuhusu chanzo cha Corona

Balozi wa China mjini London, ametahadharisha kwamba madai ya baadhi ya viongozi wa Uingereza kwamba virusi vya Corona vilitengenezwa katika maabara moha ya mji wa Wuhan nchini China, yatakuwa na taathira hasi kwenye uhusiano wa nchi mbili.

Liu Xiaoming aliyasema hayo Jumanne ambapo ameonya kuhusu matamshi ya kiholela ya baadhi ya wanasiasa wa Uingereza kuhusiana na chanzo cha kuenea virusi vya Corona kuwa ni maabara ya mji wa Wuhan, na kusema kuwa suala hilo linatia sumu kwenye uhusiano wa nchi mbili. Ameongeza kuwa, kuingiza siasa kwenye suala la virusi vya Corona, kunaondoa hali ya kuaminiana na ushirikiano wa Beijing na London. Baadhi ya wabunge wa Uingereza wamechukua msimamo sawa na wa serikali ya Rais Donald Trump wa Marekani kwa kuituhumu China kuwa inahusika katika kuenea virusi vya Corona.

Mike Pompeo, Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani pia amekuwa akidai kuwa kuna ushahidi usio na shaka kwamba virusi vya Corona vilianzishwa katika maabara moja ya mji wa Wuhan nchini China. Hii ni katika hali ambayo intelejensia za Marekani zimeeleza kuwa, virusi hivyo angamizi havijatengenezwa na mwanadamu. Aidha Shirika la Afya Duniani (WHO) limeyataja madai hayo ya Marekani kuhusiana na chanzo cha virusi vya Corona kuwa ni dhana tu na kuongeza kuwa, hakuna nyaraka wala ushahidi wa kielimu unaothibitisha kuwa virusi hivyo vimetengenezwa na China.

Post a Comment

0 Comments