Maisha yaanza kurudi upya barani Ulaya

Mamilioni ya watu barani Ulaya wanaanza kurudi kwenye maisha ya kawaida, baada ya wiki kadhaa za kujifungia ndani kwa khofu ya maambukizo ya virusi vya korona lakini wanakaribishwa na dunia ambayo si kama walivyoiwacha.
Anga la rangi ya buluu linawakaribisha wakaazi wa mji mkuu wa Italia, Rome, katika dunia ambayo kamwe haitakuwa tena ile waliyoiwacha wiki kadhaa nyuma wakati walipolazimika kujifungia ndani kwa khofu za maambukizo ya virusi vya korona. Kuna mengi yaliyobadilika na ambayo huenda yasirejee tena kwenye hali ya zamani.
Italia, taifa la pili baada ya Marekani kwa kuwa na vifo vingi vya wagonjwa wa COVID-19, limeanza rasmi shughuli za uzalishaji mali siku ya Jumatatu (4 Mei) kwa kufunguwa viwanda na maeneo ya ujenzi.
Mikahawa nayo imefunguliwa, lakini kwa huduma za kuchukuwa tu chakula, huku mabaa na maeneo mengine ya starehe yakiendelea kufungwa.
Watu wanashauriwa kuepuka kutumia usafiri wa umma, na wachache wanaoutumia, wanalazimika kuvaa barakoa.

Post a Comment

0 Comments