Makosa yanayowakwamisha watu wengi kufanikiwa

Mara nyingi tumekuwa tunafanya mambo yetu kana kwamba tuna muda mwingi sana. Kwamba kesho nayo siku, hili ni kosa kubwa sana.

Iwe unafanya kazi au unafurahia, kuwa makini na jinsi unavyotumia muda wako ni moja ya mambo mazuri zaidi unayoweza kufanya maishani mwako. Yafuatayo ni mambo  yanayoongoza kwa kupoteza muda ambayo inabidi uyaache.

Kukimbia changamoto
Iwe isiwe, utajikuta umefika mahali ukakosa pa kukimbilia mambo yatakapokufikia shingoni. Kabili changamoto zote unazokumbana nazo na uachane nazo moja kwa moja ukiwa umeshapata suluhisho zake. Kuendelea kuzikimbia haimaanishi umezitatua, zitarudi tena kwa namna tofauti.

Kulaani unapokutwa na matatizo
Sote tunakumbana na ugumu wa maisha pamoja na kushindwa kwa kiasi fulani, lakini unapoielekeza akili yako kwenye kutafuta ufumbuzi hata uwe ni wa kiwango kidogo namna gani unakuwa umeingia kwenye mchakato wa kujitoa kwenye mtego wa matatizo hayo.

Kujidanganya
Usemi kwamba ukweli unakuweka huru ni sahihi kabisa. Imani pamoja na mawazo yanayozuia uwezo wako wa kuwa na machaguo mengi zaidi hayawakilishi ukweli wako juu ya mambo au matatizo fulani na yanayofanya ni kukuzuia usitimize malengo uliyojiwekea katika maisha.

Woga
Ni jambo la asili kwa binadamu kuwa na woga na wengi wetu tunajikuta tukiogopa mambo mengi kwa sababu hatuyajui kabisa au hatuyajui vizuri. Kama ukiweza kuelewa sababu za woga ulionao, ni rahisi kujiweka huru baada ya hapo.

Mawazo hasi
Ikiwa unajiwekea malengo yako binafsi, yaweke ukiwa na tamaa kubwa ya kuyatimiza pamoja na kuwa na mtazamo chanya badala ya kufikiria mambo yatakayokushinda au yatakayokuwa vikwazo kwenye safari ya kutimiza malengo yako. Mawazo yetu yanaweza kutusababisha tufanikishe malengo tuliyojiwekea na kutufanya kuwa na furaha au kutufanya tushindwe hata kuchukua hatua ya kwanza ya kuyatimiza na kufanya tuishi kwa woga na majuto maisha yote.

Kuamini jambo ‘haliwezekani’
Miongoni mwa maadui wakubwa kabisa wa mafanikio ya jambo lolote lile ni kutojaribu kabisa au kujaribu jambo na kuliacha mara ya kwanza kabisa unapoona dalili za vikwazo. Watu wengi sana duniani wamelizoea neno “haiwezekani” kiasi cha kuwafanya waone matatizo tu kwenye kila fursa inayojitokeza.

Kufanya kazi kwa ubabaishaji
Mafanikio kwenye jambo lolote yanakuja baada ya kuwekeza muda wa kutosha, kufanya kazi kwa bidii ndani ya muda huo ili kutimiza malengo uliyojiwekea pamoja na kufanya kila lililo ndani ya uwezo wako ili kufanikisha malengo yako. Kwenye maisha, kama utakuwa tayari kutimiza majukumu yako kwenye kazi fulani – mafanikio yana namna yake ya kuja kutokana na kazi iliyofanywa vizuri.

Tabia ya ubinafsi
Maisha ya watu wengi wenye mafanikio makubwa duniani yametawaliwa na kutoa sadaka, kutumia mali zao kwa kuwanufaisha wengine pia pamoja na kusifu na kuwa karibu na watu waliokuwa na mchango mkubwa kwenye mafanikio hayo – si kupoka wengine mali zao, kulalamika na kukashifu.

Tabia ya kukosoa kila jambo
Ni rahisi sana kuwa mkosoaji, unachotakiwa kufanya ni kuangalia jambo baya kwenye kila linalofanywa – na utalipata. Kutoa sifa sahihi ni jambo lenye nguvu, lenye manufaa na kuongeza morari kwa kila anayeguswa na sifa nzuri hizo.

Kujilinganisha na wengine
Kumbuka kwamba kila mmoja anakumbana na matatizo na changamoto zake na wanapambana nazo kwa njia na nyenzo walizonazo kwa wakati huo. Acha tabia ya kujilinganisha na watu wengine kwakuwa kufanya hivi hakukusaidii kufanya jambo lolote la maendeleo.

Kughairisha mambo
Hakuna jambo linalochangia sana kupoteza muda wa mtu kama anapojikuta anaghairi kufanya mambo aliyojipangia jambo hili linaongeza msongo kwa mtu na kukupunguzia uwezo wa kuwa na machaguo mengi katika kutatua changamoto unazokumbana nazo katika maisha.

Kutaka kuwa sahihi wakati wote
Kumbuka kwamba wale wasiokosea hata mara moja ni wale wasiojaribu jambo lolote hata mara moja. Achana na mtego huu wa kutaka mambo yasiwe na dosari wakati wote. Badala ya kutafuta jambo lisilo na dosari la kufanya, kwa muda ulionao – fanyia kazi kuboresha jambo fulani mpaka lisiwe na dosari zilizokuwapo awali.
Kifupi ni kwamba hakuna anayejua atakuwa na muda wa kufanya mambo mengi ya maana kiasi gani akiwa na uthubutu wa kuachana na tabia ambazo zinachofanya maishani mwake ni kumpotezea muda. Zipunguze tabia hizi ili kuona tofauti ya maisha.

Post a Comment

0 Comments