Mambo 6 ambayo Mjasiriamali anatakiwa kuyafanya kila siku

Kati ya kitu ambacho kila mjasiriamali mwenye nia ya kufanikiwa anacho ni kule kutaka kuona anakifikia mafanikio makubwa ya kibiashara. Lakini pamoja na kuwa na nia hiyo ya kufikia mafanikio hayo, mjasiriamali huyu hawezi kufanikiwa mpaka ajue mambo ya msingi yanayoweza kumsaidia kufanikiwa na kuyafanya karibu kila siku.

Kwa mjasiriamali yoyote atakayeelewa mambo hayo itamsaidia sana kuweza kufikia mafanikio makubwa anayohitaji. Kwa kujifunza kupitia makala haya, itakuonyesha mambo ya wazi ambayo unatakiwa kuyajua kama mjasiriamali na kuyafanya kila wakati ili kuweza kufanikiwa. Sasa twende pamoja kuweza kujifunza mambo unayotakiwa kuyazingatia kila siku katika safari yako ya mafanikio.

1. Panga siku yako mapema.
Ni rahisi sana siku yako kuwa ya mafanikio ikiwa utaipangilia mapema. Ni vizuri ukaipangilia siku yako mapema ikiwezekana siku moja kabla ili kuweza kujua ni kitu gani utakachokifanya kesho. Hiyo itakusaidia kuweka malengo na kupanga mikakati muhimu ya kutekeleza mapema kichwani mwako kwanza.

Kwa mfano usiku kabla hujalala andika kwenye kitabu chako ni nini utachokwenda kufanya kesho. Kwa kufanya hivyo kila siku itakusaidia kufanya mambo mengi kwa urahisi na bila kupoteza muda hovyo. Acha kulala na kuamka kiholela. Unaweza ukaona ni jambo kama dogo, lakini lina msaada mkubwa sana katika safari yako ya mafanikio na ni muhimu kufannya hivi kila siku.

2. Amka asubuhi na mapema.
Siku zote jifunze kuamka asubuhi na mapema. Unapoamka asubuhi na mapema inakusaidia sana kukamilisha zile kazi ngumu ambazo unatakiwa uzifanye kwa siku husika. Kuamka asubuhi na mapema ni muhimu hiyo yote ni kwa sababu akili yako inakuwa bado na nguvu kubwa ya kutenda mambo mengi na kwa ufanisi mkubwa bila kuchoka.

Unaweza ukaamka asubuhi na mapema ukajisomea. Kama wewe ni mwandishi unaweza ukaamka asubuhi na mapema ukaandika au ukapitia malengo yako. Kwa kuamka asubuhi na mapema itakusaidia sana kama mjasiriamali kukufanikisha kwa sababu mipango yako mingi unaweza ukaifanya asubuhi na mapema hata kabla jua halijazama.

3. Anza siku yako kwa kuwa chanya na maliza ukiwa chanya.
Amka asubuhi kwa kujifunza kuwa chanya. Hiyo itakuwa rahisi kwako ikiwa utajisomea kitabu au utasikiliza kitabu cha sauti kupitia simu au redio. Unapoianza siku yako ukiwa chanya utaifanya siku yako iwe nzuri zaidi. Mambo yako mengi utayafanya kwa hamasa kubwa. Kitu pekee kitakachokufanya uwe hivyo ni kwa sababu uliianza siku yako ukiwa chanya.

Lakini si hivyo tu, kama ulivyoanza siku yako chanya ndivyo unatakiwa uimalize kwa namna hiyo. Imalize siku yako kwa kujikumbushia tena malengo yako. Imalize siku yako kwa kujisomea kitabu cha mafanikio hata kwa dakika kumi na tano. Hivi ndivyo unavyoweza ukawa chanya kwa siku yote na itakusaidaia kuwa mjasiriamali wa mafanikio.

4. Tunza na thamini muda wako.
Muda ni kitu cha thamani sana kwa mjasiriamali yoyote. Muda ndio unaotufanya tufanikiwe ama tusifanikiwe. Matumizi ya muda sahihi yanahitajika sana katika kila eneo la maisha yetu kuliko wengi wanavyofikiri. Hivyo kwa maana hiyo ni muhimu sana kuthamini muda tulionao na kufanya yale yaliyo ya muhimu kwetu.

Kama ulikuwa ni mtu wa kupoteza muda, achana na hiyo tabia mara moja. Sasa unatakiwa kuishi maisha ya kimafanikio kwa kuthamni na kutunza muda wako sana. Usikubali mtu yoyote akakupotezea muda wako. Wajasirimali wengi wenye mafanikio wanatunza sana muda wao. Kama lengo ni kuwa mjasirimali wa mafanikio ni vyema kujifunza kutunza na kuthamini muda sana kila siku.

5. Jiwekee lengo la kusonga mbele kila siku.
Mjasiriamali mwenye mafanikio lengo lake kubwa ni kusonga mbele. Haijalishi unakutana na nini? Lakini ukiwa kama mjasirimali unayetaka kufanikiwa thamani kuendelea mbele. Acha kuganda na kung’ang’ania sehemu moja ulipo  hiyo haitakusaidia sana. Kikubwa uwe mtu wa kusogea hatua kwa hatua kila siku.

Najua kuna wakati tunakutana na changomoto nyingi sana. Pamoja na changamoo hizo zichukulie kama ngazi ya kukupandisha kwenye mafanikio yako. Lakini ikiwa utakubali kukaa chini nakutulia basi elewa wewe mwenyewe utakuwa umeamua kuyapoteza maisha yako bila kujua. Tambua kusonga mbele liwe ndilo lengo lako la kwanza kama mjasiriamali unayetaka mafanikio makubwa.

6. Jifunze kila siku.
Yafanye maisha yako kila siku yawe shule. Kila unachopitia iwe changamoto au kile kizuri unachokiona kutoka kwa watu wengine kifanye kiwe sehemu ya darasa kwako la kukutoa kutoka sehemu moja kwenda sehemu nyingine. Andika yale mambo ya msingi ambayo unaweza ukawa umejifunza na kisha yafanyie kazi kila siku. Hapo itakusaidia sana kuwa mjasiriamali wa mafanikio.

Naamini kwa kujifunza mambo hayo, yatakuwa msaada kwako wewe kama mjasiriamali kuweza kufanikiwa kwa kile unachokifanya katika maisha yako. Kumbuka kuchukua hatua na kufanyia kazi kile ulichojifunza.

Post a Comment

0 Comments