Mambo ya kufanya hasa pale unapokutana na ugumu wa kushindwa katika maisha yako


Kushindwa na kufanya  makosa ni sehemu muhimu ya maisha yetu kama vile ilivyo hewa,chakula,na maji. Sote tunafahamu kwamba;Tunahitaji hewa safi, chakula bora, na maji safi ili kwa pamoja tuweze kuendelea kuishi.Na ndivyo hivyo pia katika kutafuta na kusaka mafanikio, kwani kunahitajika kushindwa pamoja na kufanya makosa.

Wakati Unapokuwa katika safari yako ya kuelekea katika mafanikio, ni jambo lisiloepukika kwamba;ni lazima utakumbana na makosa kadha wa kadha pamoja na kushindwa kuliko  kwingi.Na katika hali  ya namma hiyo ndipo unapokusudiwa kuweka juhudi na umakini zaidi kwenye kushikamana na ndoto na malengo yako, kwani kama usipokuwa makini, itapeleka wewe kukata tamaa, na hivyo kusababisha kufa kwa ndoto na malengo yako.

Watu wote wenye mafanikio hapa duniani, ni watu ambao kwa namna moja au nyingine walifanya makosa. Na wanatambua kwamba kushindwa na kufanya makosa  ndio huamua hatima ya mafanikio yako. Kabla haujafikia ngazi yoyote ile ya mafanikio unayoitaka katika maisha,ni lazima utafanya makosa na kushindwa kwingi hasa kabla na hata mara baada ya kufanikiwa.

Safari ya kutafuta na kusaka mafanikio kamwe haitoweza kuwa rahisi. Na kwa maana hiyo, badala ya kuruhusu kukatishwa tamaa kwa makosa na kushindwa kwako,ni muhimu ukawa mvumilivu kwa kuweka juhudi na umakini zaidi katika ndoto na malengo yako. Hakuna kitu cha thamani kubwa katika maisha kinachopatikana kirahisi rahisi.

Na kwa wakati wowote ule unapohisi kuwa upo chini au mwenye kukata tamaa,basi  ni muhimu ukatambua na kufahamu mambo haya machache...

Moja, kamwe haupo peke yako.
Ni muhimu ukatambua kwamba siye wewe pekee ndiye unayefanya makosa. Mahali fulani  na kwa wakati fulani,ukweli ni kwamba; kuna mamilioni ya watu kadha wa kadha ambao kwa namna moja au nyingine wamekuwa wakifanya makosa katika maisha. Na kwa maana hiyo badala ya kujutia kutokana na kushindwa kwako na makosa uliyoyafanya, litakuwa ni jambo la busara na hekima kama utaamua kujifunza kutoka kwenye makosa na kushindwa kwako, Na kisha ukaamua kusonga mbele.

Mbili; kamwe haupo katika hali ngumu na iliyo mbaya zaidi.
Ni muhimu ukatambua kwamba kamwe haupo katika hali ngumu na iliyo mbaya zaidi. Kwani kwa upande mwingine kunaweza kuwa na watu kadha wa kadha ambao kwa namna moja au nyingine wanaweza kuwa wapo katika hali  ngumu na iliyo mbaya zaidi kuliko yako. Na kwa maana hiyo, kufanya makosa na  kushindwa kwako kamwe hakupaswi kuwa sababu ya wewe kutokuchukua hatua kwa mara nyingine kwa kujaribu tena na tena.Tofauti kuu iliyopo kati ya wanaofanikiwa na wasiofanikiwa ni ile hali ya kuwa watu wa vitendo.Watu wenye mafanikio wanatambua kile  wanachopaswa kufanya na wanachukua hatua.

Na kwa upande wa watu wasiofanikiwa,wao huwa wanatambua kile wanachopaswa kufanya, ila kwa kutambua ama kutokutambua huanza kujipa sababu kadha wa kadha za kwanini wanashindwa kufanya kile wanachopaswa kufanya.Lakini licha ya hilo ,jambo la muhimu na la msingi kwako ni kuchukua hatua.Utafiti unaonyesha kwamba;Ni asilimia moja ( 1%) tu ya watu wote ndio hasa uchukua hatua,na watu hao wanaochukua hatua ndio hasa ufanikiwa katika maisha.Chukua hatua sasa na kamwe hupaswi kukatishwa tamaa kwa kushindwa na makosa unayokumbana nayo.

Tatu, kushindwa na kufanya makosa kamwe sio mwisho wa safari.
Wakati tunapojiwekea ndoto na  malengo yetu ndio wakati ambao wengi wetu huwa tunakuwa ni wenye  hamasa na matumaini makubwa kuhusiana na maisha yetu.ila tatizo linakuja kutokea wakati tunapokumbana na changamoto pamoja vikwazo vya kila aina.

Na vikwazo au changamoto hizo kwa namna moja au nyingine vyaweza kutupilia mbali matumaini yetu kuhusiana na ndoto  pamoja na malengo tuliyojiwekea. Hiki ni moja ya kipindi kigumu sana kwa wengi wetu. Lakini licha ya hilo kamwe hatupaswi kupoteza matumaini. Kwani kushindwa na kufanya makosa sio mwisho wa ulimwengu.

Nakutakia utekelezaji mwema kwa kile ulichojifunza. Na Kamwe usisite kuwaalika na wenzako ili nao waweze kujipatia mambo haya mazuri yenye kuelimisha na kuhamasisha.

Post a Comment

0 Comments