Obama: Hatua za Trump katika janga la COVID-19 'ni maafa kamili yasiodhibitika'

Rais Donald Trump (kushoto) akisalimiana na Rais Barack Obama (katikati ) na Makamu wake Joe Biden siku alipokuwa anaapishwa kuwa Rais wa 45 wa Marekani katika Bunge la Marekani Washington, Januari 20, 2017.

Rais wa zamani wa Marekani Barack Obama amesema Rais wa sasa wa Marekani Donald Trump jinsi anavyoshughulikia suala la janga la virusi vya corona ni maafa kamili yasiokuwa na udhitibiti. 

Katika mkutano kwa njia ya simu na wafanyakazi wake wa zamani, Obama amesema, “imekuwa ni maafa kamili yasiokuwa na udhibiti wakati fikra ya ‘nini kinanisaidia mimi katika janga hili’ na ‘sijali kinacho waathiri watu wengine’ – fikra kama hizo ndio zinatawala katika serikali yetu.”

Marekani inaongoza kwa maambukizi na vifo vinavyotokana na virusi vya corona duniani. Zaidi ya watu milioni 1.3 nchini Marekani wana maambukizi na idadi ya waliokufa inakaribia 80,000.

Huko New York, ambako ni chimbuko la mlipuko, Gavana Andrew Cuomo amesema Jumamosi kuwa watoto watatu wamekufa na wengine zaidi ya 70 ni wagonjwa wanaoonyesha wana dalili za virusi hivyo.

Watoto hapo awali ilidhaniwa kuwa hawako katika kundi hatari la maambukizi ya virusi, lakini ripoti zinaanza kujitokeza zikionyesha hilo si sahihi.

Kama ilivyo katika nchi nyingine, Marekani haina vifaa vya kutosha vya kupima virusi vya corona, ikimaanisha kuwa watu walio katika hali mbaya ya maambukizi ndio wanapimwa na wale wenye dalili hafifu kuchukuliwa vipimo baadae, jambo linaloongeza uwezekano wa wale wenye dalili za awali au wasio na dalili wanaweza wasipimwe kabisa na hivyo kutohesabiwa.

Wakati akishinikiza kufungua shughuli za kawaida Marekani kwa hatua mbalimbali zinazokusudiwa kupunguza maambukizi ya virusi vya corona, Rais Donald Trump hivi karibuni amekuwa akihamasisha mfumo wa upimaji nchini Marekani. Lakini mfumo huo umekosolewa kwa kufeli katika wiki za kwanza za dharura zilizokuwa na maambukizi na bado una mapungufu ukilinganisha na mifumo ya upimaji ya nchi nyingine.

ADVERTISEMENT


Post a Comment

0 Comments