Rais wa Kenya abadilisha uongozi wa Jubilee

RAIS wa Kenya, Uhuru Kenyatta amebadilisha viongozi wa chama chake cha Jubilee katika Baraza la Seneti. Aliyekuwa kiongozi wa wengi Kipchumba Murkomen na mnadhimu Susan Kihika wamevuliwa nyadhifa zao.

Kwenye taarifa kwa vyombo vya habari, Kenyatta alisema hatua hiyo inalenga kukiimarisha chama hicho, lakini wachambuzi wanasema ulinuia kumvunja nguvu naibu wake William Ruto.

Kikao hicho kilifanyika mapema asubuhi katika Ikulu ya Nairobi na kuhudhuriwa na maseneta 20 wa vyama vya Jubilee na KANU huku maseneta 19 wanaogemea upande wa makamu wa rais wakikosa kuhudhuria. Wakati wa mkutano huo mkuu wa maseneta, Samuel Poghisio seneta wa jimbo la Pokot Magharibi alichaguliwa kuwa kiongozi wa wengi katika bunge la seneti.

Poghisio anachukua nafasi ya seneta Kipchumba Murkomen ambaye anaegemea upande wa makamu wa rais William Ruto.

Inaaminika kuwa cheche zake dhidi ya rais Kenyatta zilichangia kumuondoa kwenye wadhfa huo. Siku chache zilizopita aliikosoa serikali ya rais Kenyatta kwa kuweka uwongozi wa kijeshi katika jimbo la Nairobi.

Seneta Irungu Kang’ata wa jimbo la Murang’a atakuwa mnadhimu wa walio wengi katika baraza hilo la Seneti. Anachukua mahala pa seneta Susan Kihika ambaye amekuwa akiandamana na makamu wa rais William Ruto kwenye mikutano ya hadhara ya kisiasa.

Seneta Fatuma Dullo wa jimbo la Isiolo anachukua wadhfa wa naibu kiongozi wa wengi katika baraza hilo la bunge.  Kimani Icungwa ni mbunge wa Jubilee na pia mwenyekiti wa kamati ya bajeti bungeni.

“Kama rais wa jamhuri ya Taifa la Kenya, anastahili kuangazia vitu vinavyomgusa mwananchi wa kawaida. Vitu anavyovifanya kwa sasa, vinalenga kumnufaisha tajiri na kikundi cha wanasiasa, sio kwa maslahi ya wakenya,” alisema Ichungwa.

Ujio wa maseneta  wa chama cha Kanu unajiri siku chache baada ya chama hicho kufanya mkataba wa ushirikiano na chama cha Jubilee. Aidha unaongeza nguvu idadi ya maseneta na wabunge wanaoegemea upande wa rais kwenye mabaraza mawili ya bunge.

Wabunge wanaogemea upande wa naibu wa rais William Ruto wamekuwa wakimtaka rais aandae mkutano wa viongozi wote wa chama hicho, ili kupiga msasa masuala yanayokiyumbisha chama hicho tangu mwaka 2017. Oscar Sudi, ni mbunge wa Jubilee.

Kwa mujibu wa wachambuzi wa masuala ya siasa mabadiliko hayo yanalenga kuvunja mbawa za makamu wake William Ruto ambaye inadaiwa amekuwa na uchu wa uongozi kiasi cha kukaidia maagizo yake ya rais.

Mfano unaotolewa ni kwamba wakati rais akijikita katika kufikia malengo yake ya maendeleo na kuonya kuhusu kampeni za mapema, makamu wake Ruto ameoneokana akizuri maeneo mbali mbali ya nchi kujipigia debe, kabla ya mlipuko wa Covid-19 kusimamisha shughuli za siasa.

Kwenye mtandao wake wa Twitter, makamu wa rais aliandika kuwa wakenya wanastahili kuungana kuwasaidia waathiriwa wa mafuriko pamoja na wale wanaokabiliwa na njaa wakati huu wa amri ya kutotoka majumbani.

Wakati huo huo kiongozi wa Chama cha Wiper Kalonzo Musyoka alisema kuwa mipango iko mbioni ya kuungana na chama cha Jubilee kwa ajili ya uchaguzi mkuu ujao.

Huku hayo yakijiri, kiongozi wa upinzani Raila Odinga alikuwa anafanya mkutano wa faragha na baraza la uongozi wa chama hicho. Ajenda ya mkutano huo haijafahamika, ila duru zinasema kuwa huenda wanajadili kuhusu muungano mpya kati ya chama cha Kanu na Jubilee pamoja na mustakabali wao.


ADVERTISEMENT

Post a Comment

0 Comments