Umeme wa SGR kukamilika mwishoni mwa Mei, 2020

Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani amesema mradi wa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme utakaotumika katika Reli ya kisasa ya kuendesha Treni inayotumia umeme umekamilika kwa zaidi ya asilimia 94 na utakamilika mwishoni mwa mwezi Mei 2020.

Dkt. Kalemani alisema hayo mkoani Morogoro , alipofanya ziara ya kukagua ujenzi wa miundombinu ya njia ya kusafirisha umeme mkubwa, na kusema kuwa ameridhishwa na kasi ya ujenzi huo ambao unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi huu pamoja na kutembelea Kiwanda cha Sukari Mtibwa kuona hali ya upatikanaji wa umeme.


Alisema Kukamilika kwa mradi huo kutachangia kwa kiasi kikubwa uchumi wa nchi kwa kuongeza mapato kwa kuwa umeme mwingi utakuwa ukinunuliwa kutoka Shirika la Umeme nchini (TANESCO), vilevile Shirika la Reli nchini( TRL) litapunguza gharama za kununua mafuta ya kuendesha treni.

Njia hiyo ya umeme itapita katika vituo vinne vya njia ya treni ya kisasa ambavyo ni Pugu mkoani Dar es salaam, Ruvu mkoani Pwani, Kidugaro na Kingulwira mkoani Morogoro.

“Mradi huu utakamilika ndani ya muda uliopangwa, kwa sababu tayari nguzo kubwa za umeme 450 kati ya 455 zinazotumika katika ujenzi wa njia hiyo, zimekwisha jengwa na kusalia nguzo tano(5) tu ambazo zinaendelea kujengwa ili kukamilisha ujenzi, hivyo kabla ya mwisho wa mwezi huu, mkandarasi atakuwa amemaliza kazi yote, na kitakachofuata ni kusubiri kukamilika kwa reli yenyewe ili tuanze kufanya majaribio ya umeme huo”, alisema Dkt.Kalemani.


Alisema kuwa mradi huo ni wa kwanza kwa nchi za Afrika Mashariki,ukifuatiwa na Kenya ambayo imepanga kuanza kuujenga mwakani 2021,na Uganda ambayo imepanga kuanza kujenga mwaka 2025.

Mradi huo umegharimu zaidi ya shilingi za kitanzania Bilioni 72.6, na mkandarasi amekuwa akilipwa fedha zake kwa wakati.

Akiwa katika Kiwanda cha Sukari Mtibwa, Dkt. Kalemani alisema kuwa serikali imetenga shilingi za kitanzania Bilioni 1.2 kwa ajili ya ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme utakaokuwa ukitumiwa na kiwanda cha sukari peke yake, katika kuendesha shughuli za uzalishaji.

Njia hiyo ya umeme inatarajiwa kukamilika ndani ya miezi sita kuanzia mwezi Mei mwaka huu, ambayo itasaidia kiwanda hicho kupata umeme mwingi na kutosha kukidhi mahitaji ya kiwanda na ziada kwa zaidi ya miaka
mitano ijayo.

“Kilichonileta hapa ni kuwajengea njia ya umeme wenu peke yenu, tumeshakaa na wataalam ili kumaliza tatizo hili, umeme hapa unatoka Msamvu takribani Kilomita 100 na unatumiwa na watu wengi, fedha tayari imekwisha tengwa na ujenzi utanza keshokutwa (Mei 13,2020) ili kukidhi mahitaji yenu ya kutaka umeme takribani Megawati 27 kwa miaka 5 ijayo, sasa lazima tuwape zaidi bila shaka mtatanua kiwanda hichi hapo baadaye,” alisema Dkt. Kalemani.

Kwa sasa kiwanda cha sukari Mtibwa kinapata Megawati 5 hadi 8 ambao pia wakati mwingine unakuwa na nguvu ndogo kutokana na kusafiri umbali mrefu pia umekuwa ukikatika kusababisha uharibifu wa vifaa na kutokidhi mahitaji ya uzalishaji.

Kiwanda hicho lilijengwa mwaka 1954 na kuanza uzalishaji mwaka 1963 hadi sasa, kinauwezo wa kuzalisha tani 200 hadi 35 za sukari kwa siku, matarajio ni kuzalisha tani 1000 kwa siku kwa kuwa wanafanya ukarabati na kuboresha miundombinu kiwanda hicho ikiwemo umeme.


ADVERTISEMENT

Post a Comment

0 Comments