UNICEF: Yatoa ripoti ya kusikitisha kuhusu mateso ya watoto wakimbizi

Mfuko wa Watoto wa Umoja wa Mataifa (Unicef) umetoa ripoti ya kusikitisha ya mwaka 2019 kuhusu hali mbaya na mateso ya watoto wasio na makazi kutokana na mapigano katika maeneo tofauti duniani.

Ripoti mpya ya Unicef inaonesha kuwa, mwaka 2019, karibu watoto milioni 19 waliishi kwenye mazingira makugumu sana ya ukimbizi katika kona mbalimbali duniani kutokana na mapigano na majanga ya kimaumbile huku baadhi yao wakiwa wameshapitisha miaka mingi bila ya kuwa na sehemu za kuishi.

Mwishoni mwa mwaka 2019, karibu watu milioni 46 walikimbia makazi yao kutoikana na machafuko na mapigano ambapo milioni 19 kati yao walikuwa ni watoto wadogo.


Bi Henrietta Holsman Fore, Mkurugenzi Mtendaji wa Unicef amesema: "Mamilioni ya watoto wadogo wanaishi bila ya makazi katika kona mbalimbali za dunia na hawana amani wala usalama na wala watu wa kuwatunza. Wakati migogoro mipya inapozuka kama corona, watoto hao wanakuwa wahanga wakubwa zaidi. Ni jambo la dharura kwa nchi na mashirika yanayoshughulikia misaada ya kibinadamu kushirikiana katika juhudi za kuwaokoa watoto hao na kuhakikisha wanakuwa salama na wanapata fursa ya kusoma."

Kwa muijbu wa Unicef, watoto wadogo ambao ni wakimbizi katika nchi zao, hawapati hata mahitaji yao ya lazima kabisa na wanatumiwa vibaya na magenge yanayofanya magendo mbalimbali.

Ripoti hiyo ya Mfuko wa Watoto wa Umoja wa Mataifa imetolewa katika hali ambayo umaskini, ukata na matukio ya kimaumbile yanazidi kuzitesa nchi za dunia hasa za barani Afrika. Matukio mengine mabaya kwa watoto wadogo ni kama mashambulio ya kivamizi ya Saudi Arabia huko Yemen, mapigano Libya na jinai zinazofanywa na magenge ya kigaidi yanayoungwa mkono na Marekani nchini Syria.

Post a Comment

0 Comments