Vifo vya watoto wachanga vimepungua kutoka 25 kwa kila vizazi hai 1000 hadi saba kwa kila vizazi hai 1000

05/05/2020 Vifo vya watoto wachanga wenye umri wa chini ya siku 28 vimepungua kutoka 25 kwa kila vizazi hai 1000 kwa mwaka 2015/16 na kufikia saba  kwa kila vizazi hai  1000 kwa mwezi Machi mwaka huu.

Hayo yamesemwa leo  jijini  jijini Dar es Salaam na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu wakati akipokea msaada wa vifaa kinga, mabango,vipeperushi na vifaa vya  kutoa elimu kwa Umma kuhusu ugonjwa wa Corona kutoka kwa Benki ya Absa Tanzania Ltd na Shirika  la UNESCO.


Waziri Ummy alisema kupungua kwa vifo hivyo kumetokana na jitihada zilizofanywa na Mhe. Rais Dkt. John Pombe Magufuli  katika kuimarisha sekta ya afya hapa nchini hii ni pamoja na kuboresha vituo vya kutolea huduma za afya, upatikanaji wa dawa, vifaa na vifaa tiba.

“Kwa namna ya kipekee niwapongeza na kuwashukuru wakunga wote hapa nchini kwa kazi kubwa na nzuri wanayoifanya kila siku ya kuwahudumia akina mama wajawazito na watoto wenye umri chini ya miaka mitano”,.

“Pamoja na kuwa maambukizi ya Virusi vinavyosababisha ugonjwa wa Corona (COVID-19) yapo na watu wanaumwa ugonjwa huu, lakini tusisahau kuwa kina mama wajawazito wanajifungua kila siku na wakunga  wanaendelea kuwahudumia kinamama hawa”, alisisitiza Waziri Ummy.

Waziri huyo aliwahakikishia wananchi kuwa pamoja na kuwa ugonjwa wa Corona upo   huduma zingine zinaendelea kama kawaida  katika vituo vituo vyote vya kutolea huduma za afya zikiwemo huduma za kliniki za akina mama wajawazito na watoto, upimaji wa magonjwa mbalimbali pamoja na upasuaji.

“Ninawashukuru wadau mliotoa vifaa hivi, ninawaomba wadau wengine waendelee kuiunga mkono Serikali katika kupambana na ugonjwa wa Corona ambao ni janga la Dunia”,.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa wizara  hiyo Prof. Mabula Mchembe alisema  vifaa hivyo vitaboresha  utoaji wa huduma za afya katika vituo vilivyopo Dar es Salaam pamoja na maeneo mengine nchini.

“Ninawahakikishia wananchi pamoja na wadau mliotoa vifaa hivi kuwa  vitatumiwa na wataalamu wetu katika kutoa huduma mbalimbali za matibabu kwa wagonjwa wanaotibiwa katika vituo vyetu vya afya”, alisema Prof. Mchembe.

Akikabidhi vifaa hivyo Mkurugenzi wa Rasiliamali watu wa benki ya Absa Tanzania Ltd. Patrick Foya alisema vifaa kinga walivyovitoa vyenye thamani ya milioni 20 ambavyo ni glovu, barakoa na vitakasa mikono vitawasaidia watoa huduma za afya wakati wanawahudumia wagonjwa.

Post a Comment

0 Comments