WHO: Amerika Kusini imekuwa kitovu kipya cha janga la corona

Shirika la Afya Duniani (WHO) limesema Ijumaa kwamba Amerika Kusini imekuwa kitovu kipya cha janga la virusi vya corona, huku idadi ya maambukizi pia ikiongezeka katika baadhi ya mataifa ya Afrika.
Mkuu wa kukabiliana na matukio ya dharura wa WHO, Mike Ryan amesema Brazil ndiyo nchi iliyoathirika zaidi Amerika Kusini, na kwamba imeizidi Urusi na kuwa nchi ya pili yenye idadi kubwa ya maambukizi ya virusi vya corona baada ya Marekani. Data zilizokusanywa na Chuo Kikuu cha Johns Hopkins, zimedhihirisha kwamba Urusi hadi hivi sasa imerikodi maambukizi yapatayo 326,448  ya ugonjwa wa COVID-19. Na, hadi kufikia Ijumaa jioni, Marekani imeripoti maambukizi yanayopindukia milioni 1.6.
Siku ya Ijumaa kumeripotiwa maambikizi mapya 20,803, na kuifanya idadi jumla Brazil kuwa 330,890 kulingana na Wizara ya Afya nchini humo. Watu wapatao 21,048 wamefariki, ikiwa ni idadi ya sita ya juu ya vifo ulimwenguni kote, kulingana na Chuo Kikuu cha Johns Hopkins.
Soma zaidi: Maambukizi ya corona yafikia milioni 4.7 ulimwenguni
Kwa upande wa Afrika, shirika hilo limesema maambukizi ya ugonjwa wa COVID-19 yaliyothibitishwa hadi sasa yanapindukia 100,000 barani humo. Ryan amesema katika wiki iliyopita, nchi tisa za Afrika zimerekodi asilimia 50 ya ongezeko la maambukizi hayo, wakati mataifa mengine barani humo yanashuhudia kupungua kwa idadi ya maambukizi.

Post a Comment

0 Comments