Rais Trump awalenga mayaya na wanafunzi katika masharti mapya ya visa Marekani

Rais wa Marekani Donald Trump
Rais wa Marekani Donald Trump ameongeza muda wa kusitishwa kwa visa za bahati nasibu pamoja na zile za wafanyikazi wa kigeni hadi mwisho wa 2020.
Wafanyikazi wenye ujuzi mkubwa wa kiufundi, wafanyikazi wasio katika sekta ya kilimo na maafisa wakuu wa makampuni wataathirika.
Ikulu ya Marekani imesema kwamba hatua hiyo itabuni ajira kwa Wamarekani wasio na kazi kutokana na mlipunko wa corona.
lakini wakosoaji wanasema kwamba Ikulu ya Whitehouse inatumia janga la corona ili kukaza sheria za uhamiaji.

Je, ni kina nani wataathiriwa?

Katika mkutano na vyombo vya habari utawala wa rais huyo umesema usitishwaji huo utakaoendelea hadi mwisho wa mwaka huu utawaathiri watu 525,000.
Watu hao ni pamoja na 170,000 waliozuiliwa na hatua ya kusitisha visa za bahati nasibu - ambazo zinawapatia raia wa kigeni makaazi ya kudumu nchini Marekani.
Ikulu ya Whitehouse kwa mara ya kwanza ilitangaza kwamba ilikuwa inasitisha visa hizo mwezi Aprili agizo ambalo lilitarajiwa kukamilika Jumatatu.
Hatahivyo raia wa Kigeni walio na visa kwa sasa hawataathirika kufuatia sheria hizo mpya zilizotangazwa siku ya Jumatatu.
Agizo hilo pia litawashirikisha wale walio na visa aina ya H-1B, ambazo nyingi hupewa wafanyikazi wa Kihindi ambao wana ujuzi wa kiufundi.
Wakosoaji wanasema kwamba visa kama hizo zimeruhusu kampuni za Teknolojia za Silicon Valley kutoa kazi kwa raia wa kigeni wanaolipwa mishahara midogo.
Mwaka uliopita , kulikuwa na takriban watu 225,000 waliotuma maombi wakishindania kazi 85,000 zilizopo kupitia mpango wa visa za H1-B.
Agizo hilo litasitisha kwa muda Visa nyingi aina ya H-2B kwa wafanyakazi wa msimu wakiwemo wale walio katika sekta ya utalii, isipokuwa wale wa kilimo, viwanda vya chakula na watalaam wa afya.
Agizo hilo pia litawaathiri wale wanaotaka visa za muda mfupi aina ya J-1, orodha inayowashirikisha wanafunzi wa vyuo vikuu na mayaya.
Maprofesa na wasomi hawakushirikishwa katika agizo hilo.
Kutakuwa na kifungu cha kuwaruhusu baadhi ya walioathiriwa iwapo watatuma maombi.
Visa za mameneja na wafanyakazi wengine muhimu wa makampuni ya kimataifa pia zitasitishwa.

Je watu wamechukuliaje sheria hiyo mpya.

''Lengo lake ni kuwalenga watu bora na werevu na wenye thamani kwa uchumi'', alisema afisa mmoja mkuu kupitia njia ya simu.
Mark Krikorian, mkurugenzi mkuu wa taasisi ya masomo ya uhamiaji, ambayo inaunga mkono sheria kali za uhamiaji, aliambia AP: Hii ni hatua muhimu iliotekelezwa na utawala wa Trump ili kulinda kazi za raia wa Marekani.
Lakini shirika la haki za kibinadamu la American Civil Liberty lilisema: Ni utumiaji wa janga la corona kubadili sheria za uhamiaji, bila kupitia bunge la Congress.
Sera hiyo mpya pia imepingwa na biashara nyingi ambazo hutegemea wafanyakazi wa kigeni.
''Huku Uchumi ukianza kuimarika, biashara za Marekani zitahitaji hakikisho la kupata nguvu kazi'' , shirika la biashara liliandika katika barua mwezi uliopita likionya kuhusu masharti hayo.
Hiyo ina maana kwamba biashara hizo zinahitaji nguvu kazi inayohitajika kupitia talanta kutoka nyumbani na hata kimataifa.

Post a Comment

0 Comments