Migogoro ya ardhi kaa la Moto, Kufunguliwa ofisi za ardhi mikoani kwaleta ahueni

Wananchi mkoani Njombe wamelalamikia kuchelewa kusikilizwa kwa Mashauri ya migogoro ya ardhi na kupelekea kuwaathiri kiuchumi wakati wakiendelea kufuatilia mashauri yanayosikilizwa na baraza ya ardhi.

Hayo yamebainishwa na baadhi ya wananchi wanaofika katika mabaraza ya ardhi yanayosuluhisha migogoro ya ardhi mkoani Njombe ambapo miongoni mwao akiwemo Remigius Ilomo na Geofrey Msambwa wamezungumzia kero wanayoipata na Kwamba Kumekuwa Kukiwaongezea Gharama kubwa pindi wanapofuatilia mashauri yao kutokana na kesi kuahirishwa mara kwa mara.

“Kesi moja inaweza ikachukua miezi sita mpaka saba kiasi kwamba uchumi unashuka kwasababu shughuli kwenye maeneo yenye kesi zinasimama,halafu inaongeza vita mbali mbali kwasbabu watu tunabaki na chuki na hatuwezi tukagombana na wahuduma”alisema Geofrey Msambwa

Ruth Mdugo ni mkazi wa kijiji cha Imalinyi wilayani Wanging'ombe mkoani Njombe ambaye anasema kilio chake kikubwa ni kesi yake kuahirishwa mara kwa mara hatua ambayo inampa wakati mgumu kwa kuwa imekuwa ikimpa changamoto kubwa katika suala la kiuchumi.

“Kinachonisumbua ni kwasababu pesa hamna na kipindi hiki imetoka kunyesha mvua,umri huu hata pesa sina natembea kwa kuhangaika kama hivi juzi nimeondaoka nyumbani kwa mguu nimelala njiani jana,ndio nimefika jioni hapa kiuchumi kwa kweli naathirika naomba mnisaidie”alisema Ruth Mdugo

Kwa kuona tatizo hilo serikali kupitia wizara ya Ardhi Nyumba na maendeleo ya makazi imelazimika kufungua ofisi za ardhi kila mkoa kwa  Tanzania Bara ambapo shughuli zote za Ardhi zitakuwa zikipatikana mkoa husika.

Kamishina msaidizi wa Ardhi mkoa wa Njombe, Christopher Mwamasage anasema kufunguliwa kwa ofisi hizo itakuwa mwarobaini katika utatuzi wa migogoro ya ardhi ambayo imekuwa ikilalamikiwa na watu wengi kila pahala hapa nchini.

“Migogoro ya ardhi mingi ni uelea tu wa sheria utakuta mtu anauza ardhi ambayo siyo ya kwakwe,na nimeorodhesha migogoro yote mkoa wa Njombe ninaielewa ilivyo najua nitapambana nayo vipi na sio kuwa migogoro ilikuwa haishughulikiwa ilikuwa inashughulikiwa”alisema Christopher Mwamasage

Kuhusu huduma zitakazotolewa na ofisi ya Ardhi mkoa wa Njombe bwana Mwamasage amesema ni pamoja na upatikanaji wa hati za Ardhi.

“Kwa hiyo kila kitu kitaishia hapa hapa Njombe hakuna sijui utaenda Dar es Salaam,Mbeya mambo yote yataisha hapa kwa hiyo ufanisi utakuwa mkubwa na wananchi watanufaika sana”Aliongeza Christopher Mwamasage

Katika vikao vya bunge la bajeti vinavyoendelea Bungeni Dodoma Waziri wa Ardhi Ameeleza Lengo la kufungua Ofisi hizo kila mkoa ikiwa ni Hatua Mojawapo ya kupunguza migogoro ya Ardhi Hapa Nchini.

ADVERTISEMENT

Post a Comment

0 Comments