Wananchi Dodoma wamshukuru Rais Magufuli kwa kupata fidia ya kupisha ujenzi wa reli ya kisasa

Wananchi jijini Dodoma wamemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kwa kupata fidia baada ya maeneo yao kuwekwa katika orodha ya maeneo yanayopitiwa na mradi wa ujenzi wa reli ya kisasa – SGR kipande cha Morogoro – Dodoma – Singida katika Kata za Ihumwa, Mkonze na Kikuyu Kusini mkoani Dodoma, hivi karibuni Mei 2020.

Zoezi hilo linahusisha fidia za nyumba na viwanja, jumla ya wananchi 2,604 wanatarajiwa kulipwa fidia yenye thamani ya zaidi ya Shilingi Bilioni 19 katika wilaya za Dodoma, Bahi na Singida mkoani Singida ili kuwawezesha wananchi kupisha mradi. Baadhi ya wananchi wameonesha kufurahishwa na hatua hiyo na kuipongeza Serikali inayoongozwa na Rais Magufuli kwa kutimiza ahadi ya kuwalipa wananchi wote ambao maeneo yao yamepitiwa na mradi wa SGR.

Aidha, pamoja na pongezi hizo wananchi wa maeneo hayo wameahidi kuendelea kutoa ushirikiano ili kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati ili uweze kuwanufaisha katika shughuli zao za kila siku, pia wameridhishwa na tahadhari zinazochukuliwa na shirika katika kupambana na ugonjwa wa Corona.

Akiongea katika zoezi la ulipaji fidia moja kati ya wanaolipwa fidia Bwana Geogre Massawe amesema kuwa “sikutegemea kama Serikali ingelipa stahiki zao mapema, si kama walivyokuwa wakidhani maana maneno yalikuwa mengi kweli hii ni serikali ya awamu ya tano haibabaishwi wala haitetereki”.

Bwana Masumbuko Mhagama mkazi wa Muungano B amesema kuwa Shirika la Reli Tanzania limetoa ushirikiano mkubwa sana katika zoezi hili kwani wamekuwa wakiwasikiliza na kutatua changamoto wanazokutana nazo katika maeneo hayo yaliyochukuliwa.

Halikadhalika Ofisa kutoka Reli anaye shughulika na Masuala ya Jamii Bi. Marry Machungwa amewatoa hofu wananchi na kuwataka kuripoti endapo kuna changamoto za kijamii zinazowakabili wawe wazi kuwaelezea kwani wapo kwa ajili ya kutatua changamoto hizo.

Pia Shirika limetoa rai kwa wananchi wanaolipwa fedha zao kuangalia kama wameridhika na tathimini hiyo au kama hawajaridhika wanaweza wakaandika barua kwa TRC ili kuweza kuangalia tena suala hilo.

Post a Comment

0 Comments