Mhe. Rais Magufuri awashukuru Wananchi kwa maombi na shukrani kwa Mungu


Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli amewashukuru wananchi wote walioitikia wito wake wa kuomba na kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa jinsi alivyoliepusha taifa katika janga la maambukizi ya virusi vya corona hadi kufikia lilipo ni Mungu ametenda kutokana na maombi hayo.

Shukrani hizo za Mhe. Rais zimewasilishwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki jijini Dar es Salaam aliposhiriki ibada ya shukrani kwa Mungu ikiwa ni siku ya tatu ya ibada hiyo, ambapo ameitaka dunia na Jumuiya za Kimataifa kutambua kuwa kauli ya Mhe Rais Dkt John Pombe Magufuli kuwahimiza Watanzania kusali na kuliombea Taifa kuondokana na maradhi ya COVID 19 kamwe haikuwa kauli ya kupuuza kanuni za kisayansi za mapambano dhidi ya ugonjwa huo.

Ni katika kanisa kuu la Anglikana la Mtakatifu Albano shahidi, Profesa Palamagamba Kabudi anapata fursa ya kuzungumza na waamini walioshiriki Ibada hiyo ambapo amesema kwamba licha ya maambukizi ya virusi vya Corona kupungua, bado wananchi wanapaswa kuendelea kuomba huku wakichukua tahadhari ili Mungu aliyewavusha katika kipindi kigumu aendelee kusimama na Taifa la Tanzania.




Baadhi ya wachungaji wamesema Mungu alimpa Mhe. Rais Magufuli maono ya kumtanguliza yeye katika vita dhidi ya Corona kwa kuwa imani ina nguvu ya kukabiliana na jambo lolote.

Channel ten pia imezungumza na baadhi ya wananchi ambao wamesema walipokea kwa kutekeleza rai ya Mhe Rais Magufuli kwa kufunga na kufanya ibada ya shukrani ili Mungu aingilie kati kulinusuru Taifa la Tanzania na janga hilo na kwamba wataendelea kuzingatia maelekezo ya wataalam wa afya ili kujikinga dhidi maambukizi

Post a Comment

0 Comments