Ndayishimiye ashinda uchaguzi wa urais Burundi

Mshindi wa Uchaguzi Mkuu Burundi Evariste Ndayishimiye

Mgombea urais kwa tiketi ya chama kinacho tawala nchini Burundi Evariste Ndayishimiye, ametangazwa mshindi wa uchaguzi wa urais.
Tume ya uchaguzi ya Burundi, imemtangaza Jenerali Ndayishimiye kuwa mshindi wa uchaguzi huo baada ya kupata asilimia 68.72 ya kura, katika sherehe fupi kwenye mojawapo ya hoteli za kifahari, kilomita 6 kutoka mji mkuu wa Bujumbura.
Tangazo hilo limetolewa chini ya ulinzi mkali wa maafisa wa jeshi la Burundi.
Kulingana na matokeo yaliotangazwa na tume ya uchaguzi, Rwasa, ambaye alivutia umati mkubwa wa watu wakati wa kampeni, amepata takriben asilimia 24.19 ya kura huku wagombea wengine watano wakipata chini ya asilimia 5 kwa pamoja.
Matokeo rasmi yanayo muidhinisha mgombea wa chama cha CNDD-FDD, Evariste Ndayishimiye mwenye umri wa miaka 52 kuwa rais wa Burundi, yatachapishwa rasmi Juni 4.
Chama kikuu cha upinzani cha National council of Liberty CNL, chake Agathon Rwasa, kimedai udanganyifu mkubwa katika hesabu ya kura.
CNL kinadai kwamba hesabu yake ya kura inaonyesha Agathon Rwasa ameibuka mshindi wa uchaguzi huo, na kusema kwamba kitawasilisha kesi mahakamani kupinga matokeo hayo.
Mshauri mkuu wa serikali Willy Nyamitwe, ambaye ni miongoni mwa viongozi wa chama kinachotawala CNDD-FDD, ametaja hatua ya upinzani kukataa matokeo ya kura kuwa isiyo ya kidemokrasia na kukosa uajibikaji kwa taifa.
Generali Ndiyashimiye ni mmoja wa wanasiasa wenye ushawishi mkubwa sana katika chama kinachotawala, na mwenye ushirikiano wa karibu san ana rais wa sasa Pierre Nkurunziza.
Uchaguzi mkuu wa Burundi ulifanyika jumatano wiki iliyopita, baada ya kampeni kughubikwa na madai ya wizi wa kura na ambao ulifanyika licha ya kuwepo wasiwasi wa maambukizi ya virusi vya Corona.
Uchaguzi huo umeandaliwa miaka 5 baada ya kuchaguliwa tena kwa rais anayeondoka madarakani Pierre Nkurunziza kwa mhula wa tatu, hatua ambayo ilisababisha machafuko yaliyopelekea vifo vya watu 1,200 na zaidi ya 400,000 kutoroka nchini humo.

Post a Comment

0 Comments